MGOMO WA WAFANYAKAZI WATATIZA USAFIRI WA NDEGE NIGERIA


MASHIRIKA ya kutetea haki za wafanyakazi ya Nigeria yameizima gridi ya kitaifa ya umeme nchini humo na kutatiza usafiri wa ndege jana.

Haya yamefanyika baada ya mashirika hayo kuanzisha mgomo uliosababisha kufungwa kwa shule na afisi za umma baada ya kushindwa kufikia maelewano na serikali kuhusiana na mshahara wa chini kabisa wanaostahili kulipwa wafanyakazi.

Mashirika hayo mawili makuu, Nigeria Labour Congress NLC na Trade Union Congress TUC yamesema yamewaamrisha wanachama wake kususia kazi baada ya serikali kukataa kuongeza mshahara wa chini zaidi kuwa zaidi ya dola 40 kwa mwezi.

Serikali ya nchi hiyo imechapisha taarifa ikisema ina nia ya kuongeza mshahara huo wa chini kabisa na kwamba itafanya mazungumzo na mashirika hayo kila siku kuhakikisha suluhu linapatikana.

Afisi ya rais wa nchi hiyo pia imetoa wito wa mkondo wa mazungumzo kufuatwa na pande zote mbili kwa ajili ya kupatikana kwa mwafaka.

Previous Post Next Post